RIWAYA| SAFARI YA KUUSAKA MWEZI (sehemu ya 11)

“Kama mnayosema ni kweli niko tayari kuwapatia mwezi wenu.” Alijibu mfalme.
          “Tunakushukuru sana kwa kukubali, tunaomba mambo yote haya tuyakamilishe kesho asubuhi ili tuweze kurejea nyumbani… wazee wetu wanateseka.” Alimalizia Minza, ukawa mwisho wa mazungumzo yetu na mfalme.
Asubuhi ilikuwa tulivu, tayari mimi na Minza tulikwisha amka na tulikuwa tukisubiri ruhusa ya kupaa kwenda kuutengeneza mwezi wao na kuuchukua mwezi wetu.
Kikosi maalumu kiliandaliwa kwenda na sisi, walipewa agizo moja tu, kutuua endapo tungeshindwa kuuwasha mwezi wao. Pia walielezwa endapo mwezi wao ungewaka basi waturuhusu kuondoka na mwezi wetu hukohuko angani.
Sekunde chache kabla hatujaondoka Minza alimfuata mfalme akanong’ona naye jambo, hapana shaka alimweleza, “Hatutauawa tunaouwezo wa kuuwasha mwezi wowote, kokote na muda wowote!”
Sisi tulipanda katika Mapandagila yetu, askari wengi wa vijitu waliokuwa zaidi ya elfu moja wakatusindikiza, wao wakipaa kwa miili yao, nasi tukipaa kwa Mapandagila.
Minza ndiye aliyekiongoza chombo, mimi niliendelea kukisoma kitabu kilichoeleza namna ya kuuwasha mwezi uliozima. Baada ya mwendo wa masaa mawili, Minza alipunguza mwendo nikagundua kuwa tumekaribia kufika, nikakiweka kitabu changu pembeni.
Niliweza kuona miezi miwili ikiwa imekaribiana, mwezi wao haukutoa mwanga wowote hata ulianza kubadilika na kuwa mweusi. Mwezi wetu uling’ara kama tochi hata ulipotuona ukatutambua na kutoa tabasamu pana.
Tulitua katika mwezi wao, nikafukua chini taratibu kisha nikapigapiga mara kumi, nikagundua kuwa mwezi wao ulizima kwa sababu walizidisha mafuta wakati wanausafisha. Nilichukua kifaa kidogo katika Mapandagila yetu, Minza akanisaidia kubeba baruti ndogo, tukashirikiana kukizika kile kifaa na ile baruti kisha nikawaamuru wote wasogee mbali kiasi. Baada ya dakika tano, baruti ile ililipuka na kile kifaa nilichoweka kikapaa juu kisha kikarudi kwa kasi na kuzama chini umbali ambao hatukuutambua, mara ghafla mwezi wao ukawaka na kutoa mwangaza tena. Wote wakashangilia kwa furaha.
Wakiwa na furaha, nilisogea karibu yao kwa unyenyekevu mkubwa, nikaweka mikono yangu kifuani kisha  nikawaomba waturuhusu tuondoke na mwezi wetu,

Itaendelea jumapili…

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne