Dhima ya Mwanafasihi Katika Jamii
Mwanafasihi ni mtu ambaye hutumia
muda wake katika utungaji wa kazi za fasihi simulizi au andishi. Ipo mifano
mingi ya wanafasihi, miongoni mwao ni: Shaabani Robert, Theobald Mvungi, Ardin
Mtembei na wengine wengi. Mwanafasihi ana dhima nyingi katika jamii, miongoni
mwazo ni:
i.
Kuielimisha
jamii yake. Mwanafasihi mzuri ni yule anayelenga katika kuipatia elimu jamii
yake juu ya mambo mbalimbali. Shafi Adam Shafi katika riwaya ya Vuta n’kuvute,
ameielimisha jamii kwa kiasi kikubwa juu ya umuhimu wa kupigania uhuru na
kujitawala wenyewe.
ii.
Kuburudisha
jamii. Aghalabu mwanafasihi hulenga katika kuiburudisha jamii yake ili
kuiondolea uchovu wa shughuli ngumu za uzalishaji mali. Unaposoma kazi ya
fasihi, akili na mwili huburudishwa na ule ufundi wa mwanafasihi wa kusimulia
mambo. Hakuna ubishi kuwa usomaji wa kazi za mwanafasihi Kezilahabi
huburudisha.
iii.
Kuhifadhi
na kurithisha amali za jamii. Mila na desturi za jamii yetu zimehifadhiwa
katika fasihi. Mfano, riwaya ya Janga Sugu la Wazawa ni miongoni mwa kazi za
fasihi zinazohifadhi mambo mengi muhimu sana katika jamii. Mfano mwingine ni
tamthiliya ya Kinjekitile, ambayo inaelezea kwa undani mkasa wa kuzuka kwa vita
vya majimaji na jinsi ambavyo babu zetu walipambana kwa nguvu zao zote katika
vita hivyo.
iv.
Kukuza
lugha. Mwanafasihi ana kazi kubwa ya kuhakikisha lugha yake inakua. Mwanafasihi
Shakespear wa Uingereza amefanya kazi nzito
katika kuikuza lugha ya kiingereza.
Maana yake ni kwamba, kadiri lugha inavyotumiwa na watunzi, ndivyo inavyozidi
kukua na kupevuka. Shaabani Robert ni miongoni mwa wanafasihi ambao wameisaidia
lugha ya Kiswahili kukua kwa kuanzisha misamiati mipya.
Katika jadi ya ushairi wa Kiswahili inadaiwa kuwa,
ushairi ulikuwa ni ghala ya maneno. Washairi walitumia maneno magumu au
yasiyokuwa ya kawaida makusudi ili kuyahifadhi yasipotee. Katika tamaduni
nyingine, kazi hiyo hufanywa na makamusi na vitabu viitwavyo, ‘hazina za
maneno:’ Kwa kuwa Waswahili hawakuwa na makamusi, kazi ya kuhifadhi maneno
ilifanywa na ushairi. (Masebo&Nyangwine:7).