Maajabu ya Mugabe, Maajabu ya Umoja wa Afrika

Marehemu, Robert Mugabe
Robert Mugabe, baba wa taifa la Zimbabwe amepita katika nyakati nyingi kinzani. Kwanza, akiwa kama shujaa, mkombozi wa nchi yake kutoka kwa mkoloni. Pili akiwa mtetezi wa wanyonge weusi, aliyethubutu kuwanyang’anya mashamba wazungu na kuwapatia wazawa. Hili la tatu linasababishwa na jambo la pili, Mugabe akiwa madarakani anashuhudia nchi ikiporomoka kwa kasi ki uchumi, mporomoko huo unaifanya nchi hiyo ishindwe hata kutumia fedha yake!
Umoja wa mataifa ya Afrika haukuisaidia Zimbabwe katika masaibu haya. Masaibu ambayo ama kwa hakika yamesababishwa na mataifa ya kibeberu. Umoja huu butu utawezaje kuisaidia Zimbabwe ikiwa umoja huu asilimia 60 ya bajeti yake unategemea fedha za msaada kutoka hukohuko katika mataifa ya kibeberu!
Maajabu ya Umoja wa Afrika hayakuanza zama hizi, mwaka 1978 ulishindwa kuzuia vita vya Tanzania na Uganda. Na mpaka wakati huu ukitazama yanayotokea Sudan, Congo, Afrika ya Kati, Nigeria, Somalia, Libya… lazima ujiulize ni nini hasa kazi ya Muungano wa Afrika – Muungano usio na fedha…FEDHEHA!
Wiki kadhaa zilizopita, mzee Mugabe akiwa na mapenzi ya dhati na muungano huu usio na meno, aliamua kuuchangia kidogo alichojaliwa, mabepari wamebomoa uchumi wa nchi yake kwa kisingizio cha demokrasia, angetoa nini ikiwa fedha hakuna? Basi mzee wetu alitoa ng’ombe! Utoaji huu una maana kubwa, kwamba hakuna mwanadamu anayehitaji fedha kwa hakika, bali twahitaji vitu fulani ambavyo pengine vyaweza kupatikana kwa urahisi palipo na fedha. Hivyo bara la Afrika kushindwa kuendelea kwa kisingizio kuwa halina fedha ni UJUHA.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Uhakiki wa Riwaya ya Watoto wa Maman’tilie