KINACHOENDELEA TANZANIA NA HATMA YETU


“Kumbadili Waziri, hata waziri mkuu, si jambo la ajabu. Anaweza kujiuzulu, anaweza kufukuzwa na nchi isitikisike. Lakini huwezi kumtikisa Rais wa nchi bila kuitikisa nchi yenyewe.” (Nyerere, 1994:59-60).
Sisi kama wananchi wa kawaida, tunatakiwa kuwachagua viongozi wetu kwa uangalifu mkubwa, wakishachaguliwa wanatakiwa wajiheshimu na kuwa waangalifu sana. Hapana shaka Nape hakuwa mwangalifu alipopitisha sheria mbovumbovu ikiwemo kuwanyima wananchi haki ya kutazama bunge mubashara. Japo anastahili pongezi kwa uungwana aliouonesha dakika za mwisho. Hali hii ni ya kawaida kabisa kama asemavyo Jenerari ulimwengu kuwa viongozi wa kiafrika hupata akili wanapomaliza muda wa utawala wao.
Haya yanatufundisha kuwa kumbadili waziri si jambo la ajabu, mfano, hayati Mfaume Kawawa alikuwa waziri mkuu kwa muda mrefu. Hakuwa amefanya kosa lolote, lakini nafasi yake ilichukuliwa na hayati Edward Moringe Sokoine. Watu aina ya Kawawa hawapatikani kama pipi dukani, ni watu adimu na huenda huzaliwa kila baada ya miaka 100.
HATMA YETU
Viongozi wabadili mbinu, jamii imebadilika… lengo letu sote ni lilelile kuiona Tanzania ikisonga mbele kama farasi wa vita. Kwanza viongozi waepuke kuahidi mambo makubwa ambayo hawawezi kuyatimiza. Waliahidi huduma bora za kiafya, badala yake tuna vijana madaktari waliofaulu vizuri zaidi ya 2500 wako mtaani hawana ajira, serikali haina fedha! huku tukiwa na upungufu wa madaktari zaidi ya 3000. Suala la walimu na sekta nyinginezo ni ukakasi sasa kulisema.
Viongozi waepuke kutoa matamko bila kushirikisha wananchi. “Nchi hii si ya kisultani, tukianza kuvumilia masultani wa kuchaguliwa tutapanda mbegu ya masultani wa kuzaliwa.” (Nyerere, 1994:59).
Tumeshuhudia viongozi wetu wakiponzwa na matamko yao wenyewe, na wengine wakizozana na kupingana hadharani mithili ya kikundi cha wasutaji kilichombana mwongo uchochoroni.
Mwandishi Carnegie, (1936) anashadadia hoja yangu, “People are more likely to accept an order if they have had a part in the decision that caused the order to be issued.”
Mwisho viongozi walinde sura za wanachi wao, si vyema kuwatangaza, kuwatumbua wala kuwananga mchana kweupe mbele ya kundi kubwa la watu, tuitane kimyakimya, tufuate sheria, mharifu huwa haitwi mbele ya kamera zilizotangulizwa na matumbo ya waandishi wa habari. Huo ni uchuro, na matokeo ya vitendo hivi wote tumeyaona. NCHI IMETIKISIKA KWA KUIBULIWA KASHFA NZITO ZA VIONGOZI ZILIZOKOSA MAJIBU.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne